“Kumegeana mkate si kwa chakula tu, bali ni maisha yote ya taabu,
furaha, na maisha yote kimwili na kiroho”
Imani ni maisha ambayo ili yawe na maana kwetu ni lazima
tuyatafakari na kuyajadili kwa pamoja. Ni lazima kuelimishana na kupeana
mwanga, tusiamini kama Watoto wachanga bali tuamini kama watu wazima wenye
kuwajibika.
Imani ya Kikristo ina matukio makubwa mawili, {a}kuzaliwa, na
{b}kufa na kufufuka kwa Kristo. Siku chache zimepita tangu
tulipoadhimisha kufa na kufufuka kwake Kristo zaidi ya miaka elfu mbili
iliyopita.
“Alipoketi kula chakula pamoja nao, alichukua mkate akabariki,
akaumega, akawapa. Na macho yao yakafumbuliwa, wakamtambua; lakini yeye
akatoweka kati yao” Luka 24:30-31.
Luka katika sura ya 24:13-35 anaeleza kisa
cha kushangaza kidogo baada ya ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Kisa
kinatokea k atika barabara ya kwenda Emau. Labda hii ni barabara ya kiimani,
maana hata Mtume Paulo, anakutana na Kristo na kuwa mfuasi wake wa
kweli katika barabara hii.
Katika barabara hiyo, Kristo aliwatokea Wafuasi wawili, cha
kushangaza ni kuwa ndugu hawa wawili hawakuweza kumtambua japo walitembea naye
na kuongea naye kwa muda juu ya matukio mbalimbali ya Yerusalemu, na hasa tukio
la kifo cha Kristo. Wakati wote huo waliokuwa wakizungumza naye bado hawakuweza
kumtambua, upo ushahidi kuwa hata baada ya ufufuo bado Kristo alibaki katika
sura ileile, hakubadilika. Tazama maandiko katika luka 24:38-39, na Yohana
20:27.
Kutokana na ushuhuda toka katika maandiko hayo, ni kweli kuwa
Kristo alifufuka na mwili wake. Lakini wale Wanafunzi wa Emau hawakuweza
kumtambua. Inashangaza! Ila walipomkaribisha ndani kwao wakati wa chakula,
alimega mkate akaanza kuwagawia, kwa tendo hilo wakamtambua, kwa nini iwe
hivyo?
Jibu pekee la kuondoa mashaka yote ni kwamba kitendo cha kumegeana
mikate, kitendo cha kukumbuka wengine kwanza, kitendo cha kugawa chakula kwa
wengine kwanza, kilifanywa na Kristo peke yake. Hiki ndicho kitambulisho chake
kikubwa. Vinginevyo hakuna, hakuna maelezo ya wafuasi wake walioishinaye,
wakasafiri naye na kusikiliza mahubiri yake, wamsahau na kumkumbuka tu
alipoumega mkate na kuwagawia wao kwanza.
Jamii ya wakati wa Yesu na jamii yetu leo ni kuwa, mtu anakula
kwanza kabla ya kuwakumbuka wengine, ni kwamba mikono inaelekea kinywani kwanza
kabla ya kuwagawia wengine. Kila mtu anashughulikia uhai wake kwanza, kila mtu
anatafuta mali zake kwanza, kila mtu anashiba kwanza, ndiyo maana wengine
wanakula na kusaza na wengine wanalala na kufa kwa njaa!
Uhakika wa hili kwanza tunaupata pale Kristo alipofanya muujiza wa
kuongeza mikate na samaki. Mitume walikuwa na chakula chao, walitaka wale
chakula chao, na wale waumini wengine waende kutafuta chakula chao huko mjini:
“Basi Yesu aliwaita wanafunzi wake akasema, ‘nawaonea watu hawa huruma
kwasababu kwa siku tatu wamekuwa nami, wala hawana chakula. Sipendi kuwaacha
waende bila kula wasije wakazimia njiani’, wanafunzi wakamwambia, ‘hapa tuko
nyikani, tutapata wapi chakula cha kuwatosha watu wengi hivi? Yesu akawauliza
“mnayo mikate mingapi?” wakamjibu, “saba na samaki wachache”. Basi Yesu
akaamuru watu waketi chini. Akaichukua ile makate saba na wale samaki,
akamshukuru Mungu, akavimega, akawapa wanafunzi nao wakawagawia watu wote
wakala, wakashiba…” Mathayo 15:32-37.
Saba ni namba takatifu, haina maana kwamba walikuwa na mikate
saba. Kwa maneno mengine mitume walitaka kusema walikuwa na mikate ya kuwatosha
wao tuna si ule umati wa watu, lakini Yesu alitaka umati ule kwanza kabla ya
mitume na yeye.
Hapa ndipo ujumbe na upekee wa Kristo Yesu umelala; yaani
kuwakumbuka wengine kabla yako wewe! Na mkate unayachukua maisha yote. Mkate ni
chakula, na chakula kinaleta uzima. Hivyo kumegeana mkate ni kumegeana uzima!
Matatizo ya dunia yetu yamelala hapa. Ni kwamba katika hali ya
kawaida, hali ambayo haina imani ya Kimungu, kila mtu anajiangalia yeye kwanza,
ashibe yeye kwanza, kila familia inajiangalia kwanza, kila taifa linajiangalia
kwanza kabla ya kuangalia usalama wa taifa jingine kwanza. Umaskini, vita, na
taabu zote za dunia yetu ni kwamba hatutaki kumegeana mkate!
Baada ya kufundisha kwa muda wa miaka mitatu, Yesu aliwaaaga
mitume kwa fundisho ambalo linabeba ujumbe wake hapa duniani: “halafu akatwa
mkate, akashukuru, akaumega, akawapa akisema: “huu ndiyo mwili wangu unaotolewa
kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa kunikumbuka” Luka 22:19.
Walipoandika injili hawatuambii kuwa Yesu alikula kwanza.
Tunachosoma ni kuwa alimega mkate na kuwapatia kwanza. Na akawaambia
kwamba wakitaka kumkumbuka na kukumbuka mafundisho yake, wamegeane mikate!
Hata jumuiya nyingi za Kikristo zilitambuliwa kwa kitendo cha
kumegeana mikate. Hivyo na wafuasi wake wale wa Emau walimtambua tu kwa kumega
mkate, hawakumtambua kwa sura yake, sauti yake au kitu kingine.
Kila mwaka tunaposheherekea Sikukuu ya Pasaka, tunakumbwa na
mafumbo ya kufa na kufufuka na fumbo la msalaba na kuuchukua kama ishara yetu
kubwa. Tunakumbwa na utamaduni wa kufanya sherehe hii kila mwaka, ila hatuzami
katika tafakuri ya ujumbe wa Kristo ya kumegeana mikate.
Ni nani anammegea jirani yake mkate? Katika Kanisa, katika
Ushirika, katika mitaa, vipi katika familia?
MBONA MSALABA WAKO UMENAKSHIWA NA KUWEKWA DHAHABU?
Msalaba umekuwa ishara kubwa ya Kanisa. Viongozi wengi wa dini
{Wakristo} wanavaa mikufu yenye misalaba shingoni kama ishara ya Ukristo au
kumwakilisha Kristo ndani na nje ya Kanisa. Makanisa yanajitambulisha kwa
ishara ya msalaba, hata Wakristo walio wengi wanajitambulisha kwa kufanya
ishara ya msalaba kwa kila tendo jema wanalotaka kulifanya ama shukrani.
Msalaba umetolewa kwenye hali yake ya kubeba majuto na mateso na
badala yake umenakshiwa na kupambwa kwa dhahabu! Msalaba haukuwa wa dhahabu,
haukunakshiwa, ulikuwa mti tu.
Yote haya yanatendeka ama kimaksudi ama kwa kutokujua kuwa ishara ya Wakristo sio msalaba bali ni kumegeana mikate. Lakini hata kama ni lazima sana kutumia msalaba basi sio wa dhahabu!
Social Plugin