UKITAKA KUMPIKA CHURA HAI USIMUWEKE KWENYE MAJI YA MOTO, ATARUKA.


Kuna kanuni moja inaitwa ‘the law of deterioration’ kwa tafsiri isiyo rasmi ni kanuni ya uharibifu/mmomonyoko. Kanuni hii inaelezea namna uharibifu mkubwa unavyoanza kwa hatua ndogondogo sana, uharibifu/mmomonyoko huwa hautokei kwa mara moja, ama kwa ghafla.

Mmomonyoko sio lazima uwe wa udongo tu, kuna mmomonyoko wa maadili pia, yote namna inavyoanza huwa si rahisi kuona ama kupima ukubwa wa tatizo utakavyokuwa. Mmomonyoko wa udongo huanza kwa tabaka la juu la ardhi ya eneo kuondolewa kidogo kidogo na ama maji, upepo, na wanyama wanaopita eneo hilo mara kwa mara, na hatimaye korongo kubwa hutokea hapo ikiwa hapakuchukuliwa hatua za kudhibiti visababishi vya mmomonyoko huo. Na gharama za kuziba korongo huwa ni kubwa zaidi ya gharama za kuzuia viasababishi vya mmomonyoko.

Kila kitu chenye mazalisho makubwa huanza kidogokidogo.

CHURA

Tuseme mfano wa chura, unapotaka kumpika chura, usimuweke kwenye sufuria yenye maji yaliyokwisha chemka kabisa, ataruka na kukimbia, lakini chura huyo huyo unapomuweka kwenye sufuria yenye maji ya baridi na kasha kuitenga motoni chura huyo ataendelea kukaa humo huku akiendelea kujitahidi kuzoea hali ya maji yanayochemka kidogo kidogo, mwisho maji yatachemka kiasi cha chura kushindwa kustahimili joto la maji hayo, hapo ataamua kutoka nje ya sufuria ya maji ya moto lakini bila mafanikio, hatafanikiwa kutoka humo kwasababau hatakuwa na nguvu za kuruka nje kwakuwa amemaliz nguvu zake katika kukabiliana na hali ya mabadiliko ya joto la maji yaliyokuwa yakichemka kidogo kidogo, na kwa hivyo utakuwa umefauru kumpika chura akiwa hai.

Mabadiliko yeyote katika maisha ya mwanadamu bila kujali ni mazuri ama mabaya huanza kidogo kidogo, taratibu taratibu, na mwisho hukamilika.

Umaskini huanza kuja kidogo kidogo, na utajiri hali kadharika, kufilisika nako pia, uzito wa mtu huanza kuongezeka kidogo kidogo na kupungua uzito hali kadhalika. Kukua kiroho huanza kidogo kidogo, na kufa kiroho huanza kidogo kidogo, umaarufu huanza kidogo kidogo, na huisha kidogo kidogo, wawekezaji wakubwa wengi wao walianza kuwekeza kidogo kidogo, walikuwa na mtaji mdogo.

MAFANIKIO/UTAJIRI

Kuna tatizo moja tu kwa watu wali wengi, wengi wetu tunapenda mafanikio na utajiri, mafanikio ya haraka haraka, wengi wetu si wavumilivu na tunakata tama mapema na kuzitelekeza ndoto zetu njiani kwakuwa hatuwezi kuyasubiri mafanikio yanayokuja kidogo kidogo. Zipo kanuni za kufikia utajiri, zote zinahusisha hatua ndogo ndogo na uvumilivu hatimaye kufikia utajiri huo. Unaweza kufanikiwa sana kwenye biashara kwa kuanza na mtaji mdogo ulionao.

Anza na hicho kidogo ulichonacho, kuwa na subira na mvumilivu, mwishoni utapata kile kikubwa unachokihitaji, jambo lamsingi usipoteze maono yako na dira ya kule uendako hata kama itakuchukua muda mrefu kukamilika.

Usitafute njia za mkato kufikia matarajio na maono/ndoto zako, zitakupeleka pabaya, watu wengi wameingia kwenye ushirikina kwa kutaka kupita njia ya mkato kutimiza ndoto zao, wengi wamekuwa majambazi na mwishowe kufa kifo kibaya kwa kutaka kupita mjia ya mkato kufikia ndoto zao. Mali yeyote unayoipata kwa njia halali hukupa amani ya moyo, lakini mali ya udhalimu na ushirikina huwa haina amani nawe.

Anza kidogo kidogo!