JE NI KWELI UNAOGOPA KUTANGAZA NIA KWA KUHOFIA KUKATWA?


Je ni kweli unaogopa KUTANGAZA NIA kwa kuhofia KUKATWA?

Kama kweli unaogopa kukatwa basi tangaza nia. Maneno haya mawili "kutangaza nia, na kukatwa" yamekuwa ni maneno yaliyojipatia umaarufu mkubwa sana kwa siku za hivi karibuni hapa nchini kwetu Tanzania, kwa jinsi yanavyotumika na kuchukuliwa unaweza kudhani ni maneno mapya kabisa pengine hata kwenye kamusi hayapo, yamekuwa ni kama maneno ya msimu tu, lakini ukweli ni kuwa maneno haya yapo na tumekuwa tukiyatumia mara nyingi tu kwenye shughuli zetu za kila siku, nyumbani na nje ya nyumba zetu. wakati mwingine tumeyatumia moja kwa moja (directly)na wakati mwingine si moja kwa moja (indirectly), unaweza usiseme kuwa "ninatangaza nia" lakini kwa matendo yako na maneno yako fulani ukawa unatangaza nia juu ya mambo kadha wa kadha unayotaka kuyafanikisha, nia ni matamanio ama malengo; mara nyingi umetangaza nia pasipokutangaza nia.

Kitu kikubwa kinachoyafanya maneno haya kuwa na msisimko wa aina yake ni harakati na mchakato wa uchaguzi wa mambo ya kisiasa tunaoupitia muda huu nchini mwetu.

Dhamira yangu si kujadili mambo ya harakati hizi za uchaguzi na makandokando yake, nimedhamiria kuhamasisha mabadiliko ya maisha ya mtu mmoja mmoja, kwa kutumia maneno haya maarufu na kwa wakati huu maarufu.

Nitaka nikwambie kwamba, usipotangaza nia ya kutumia muda wako vizuri kubadilisha maisha yako, basi maisha haya yatakukata. Inatia huzuni sana kuona kuwa wapo watu wanaishi maisha haya pasipokuwa na malengo mahususi kwa kila dakika na saa inayopita, hawaujutii  muda wanaoupoteza kwa kukaa na kupiga porojo juu ya watia na wanaokatwa kwenye michakato ya kisiasa, na ndiyo hao wanaotegemea wanasiasa wanaokatana wawaletee maisha bora, kutwa ni kulaumu viongozi na serikali, wanashinda vijiweni kusimuliana maisha ya watu wengine(majungu), wanapoteza muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii kufuatilia maisha ya wasanii wa bongofleva na wa bongo muvi, wanatumia muda mwingi kupakua na kuposti picha na vitu vingine vingi visivyokuwa na tija kwenye maisha yao, wanatumia muda mwingi kufuatilia na kulike picha za watu wasiowafahamu, na wanatumia muda mwingi kwenye TV.

Na kibaya zaidi wanatumia fedha kidogo wanayoipata kununua vitu wasivyo vihitaji ili tu kujionesha kuwa nao wanajua matumizi. Wananunua vitu kwakuwa ndiyo fasheni, ama kwakuwa jirani na fulani amenunua.

Ndugu yangu, fedha hiyo na muda huo hautarudi kamwe saa ikipita imepita, na siku hali kadhalika, tumia huo muda kusoma kitabu kitakacholetea tofauti chanya kwenye maisha yako angalau hata ukurasa mmoja tu kila siku, na fanyia kazi hicho utakachojifunza, sikiliza CD zenye mafundisho kuhusu kazi, biashara ama kitu chochote kinachoweza kukuletea mabadiliko kwa kuboresha kazi ama hicho unachokifanya kukupatia mkate wa kila siku; badala kukaa kijiweni na watu unaolingana nao mawazo tafuta marafiki wapya wanaokuzidi hatua fulani maishani jifunze kutoka kwao, itakubadilisha sana kimaisha, usiwaonee gere na kuanza kuzusha maneno dhidi yao.

Wewe ni kiongozi na mtawala wa maisha yako, usiache vitu na watu watawale na kuongoza maisha yako.

Tangaza nia ya kutumia muda wako vizuri, na kuishi maisha ambayo hujayazoea. Tangaza nia juu ya matumizi ya simu yako, juu ya marafiki zako, juu ya vipindi unavyofuatilia kwenye TV yako.

Maisha hayatakukata ukichukua hatua hii ya KUTANGAZA NIA bali usipochukua hatua hii uwe na uhakika UTAKATWA!