Msamaria Mwema

Katika chuo kikuu fulani cha Theolojia, wakufunzi waliamua kufanya jaribio kwa wanafunzi wa uchungaji hapo chuoni. Wakawakusanya wanafunzi 40 kisha wakawaambia kwamba wanatakiwa kwenda kwa haraka sana kwenye kumbi za lekcha hapo chuoni kuelezea kisa cha Msamaria Mwema kama kilivyosimuliwa na Bwana Yesu (Luka 10:30-37) kwa wanafunzi wanaowasubiri huko, na kwamba watapimwa kwa uharaka wa kufika na umahiri wa kuelezea kisa hicho. Kwenye njia za kuelekea kwenye kumbi hizo wale wakufunzi wakaweka watu waliokua wamevalia mavazi duni sana huku wakijikohoza na kujifanya kana kwamba wanaugulia maumivu makali. Kutokana na hamu ya kufaulu mtihani na kupata uchungaji, wale wanafunzi hawakusimama njiani kutoa msaada wala kuwauliza wale mahututi njiani nini kimewasibu.

Wengi wetu tunajibidiisha kila siku ili kufikia maisha ya juu tuweze kusaidia watu wengine ili tupate baraka za Mungu. Lakini katika safari zetu hizo ni muhimu kukumbuka kwamba njiani zipo fursa za kuinua na kusaidia wengine na kupata baraka za Mungu. Wakati mwingi visababishi vya baraka za Mungu kwetu vipo njiani (wale mahututi/majeruhi) na si mwisho wa safari (chumba cha lekcha au hekaluni).

Umeshawahi kuipita ibada na baraka yako njiani wakati unaenda ibadani kubarikiwa? Soma tena Kisa cha Msamaria Mwema. Luka 10:30-37

Lazaro Kavageme 
Inuka Tuondoke Ministries 
Mwanza - Tz